17 October 2014



Kijana mmoja mkazi wa Kimandolu jijini Arusha, Paulo Simon (18) amelazwa hospitali ya mkoa Mount Meru, baada ya kubakwa na kisha kukatwa ulimi na mwanamke mmoja aliyekuwa akimtaka kimapenzi.

Tukio hilo la kusikitisha limetokea usiku wa kuamkia Jumanne majira ya saa 6.30 katika eneo la Tindigani, Kimandolu, wakati mwanamke huyo aliyetambulika kwa jina moja la mama Abuu alipofika katika baa hiyo kama mteja na baadae kumlazimisha mhudumu wa baa hiyo kufanya mapenzi bila ridhaa yake.

Simoni ambaye ni mfanyakazi katika baa hiyo, inayomilikiwa na Mwenyekiti wa Mtaa, Joel Mbasha, alisema mnamo majira usiku alikuja mwanamke huyo na kuagiza kinywaji na kumuhudumia.

Alisema ilipotimu majira ya saa 6.30 wateja waliisha na kuamua kufunga baa, hata hivyo mwanamke huyo alieendelea kunywa pombe taratibu katika eneo la kaunta.

“Mimi sikuwa na mazoea kabisa na mwanamke huyo kwanza ukimwangalia ni kama mama yangu, wakati nikifunga baa na kujaribu kuondoka alinifuata na kuniambia anataka tukafanye mapenzi nilimkataa ndipo aliponishika kwa nguvu sehemu zangu za siri,” alisema.

Alisema alipatwa na maumivu makali na kuanza kupiga kelele lakini mwanamke huyo aliendelea kumng’anga’nia sehemu zake za siri huku akimziba mdomo kwa kutumia kinywa chake na baadae alifanikiwa kumng’ata ulimi na kuutema chini.

“Alipoona napiga kelele akaleta mdomo wake kwenye mdomo wangu akanishika kichwa na kuniingizia mdomo wake huku mkono wake mmoja ameshika sehemu zangu za siri nilikuwa nasikia maumivu makali sana wakati nalia ndipo alipofanikiwa kuning’ata ulimi na kuondoka nao kisha aliutema karibu na mlango wa baa,” alisema.


Majeruhi huyo kwa sasa hali yake bado si nzuri kwani hawezi kuzungumza na muda mwingi anatokwa na damu nyingi hali iliyosababisha wauguzi katika hospitali anayotibiwa kumuwekea ndoo kutema damu.

Jeshi la polisi mkoani Arusha limethibitisha tukio hilo na kwamba mtuhumiwa anashikiliwa na upelelezi utakapokamilika atafikishwa mahakamani.

0 comments:

Post a Comment

.

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!