30 July 2012




BAADA ya kutamba kwa muda mrefu katika muziki wa kizazi kipya nchini, msanii nyota wa muziki huo, Naseeb Abdul ‘Diamond’ amesema anafikiria kujitosa katika muziki wa taarab. Diamond alisema Jijini Dar es Salaam wiki hii kuwa,amefikia uamuzi huo kutokana na kuvutiwa na muziki huo wa taarab.
 Mshindi huyo wa tuzo mbalimbali za muziki za Kilimanjaro amesema, anajua uamuzi wake huo utawashangaza mashabiki wengi, lakini ni jambo la kawaida kwa msanii. 
 Diamond alisema hadi sasa anaamini hana mpinzani katika muziki wa kizazi kipya na hakuna msanii anayeweza kufikia kiwango chake hapa nchini.
 Diamond alisema ameamua kupiga miondoko tofauti ya muziki kutokana na kipaji alichonacho katika fani hiyo, ambayo imempatia umaarufu mkubwa, Kutokana na kipaji chake hicho,Diamond alisema hakuna kitu anachoshindwa kukifanya katika fani ya muziki.
 Alisema bado hajaanza rasmi kupiga muziki wa taarab,na kuwa sasa anafanya tathmini ya soko la muziki huo ili kuona kama unaweza kumletea mafanikio kama ilivyo kwa muziki wa bongo fleva. 
 Alisema anaweza kufanya kila aina ya muziki kwa sababu anakipaji cha kuimba nyimbo aina zote, hivyo endapo atafikia muafaka anaweza kufanya muziki wa taarabu. 
 Diamond alikiri kuwa, muziki wa kizazi kipya umemfanya ajulikane sehemu nyingi duniani, ikiwa ni pamoja na kupata manufaa mbalimbali kimaisha kwa kuishi kwenye nyumba nzuri na kumiliki magari ya kifahari.


source:www.jukwaahuru.com 

0 comments:

Post a Comment

.

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!